Tuesday 5 August 2014

Jeshurun's Mind: Kiswahili na Mashairi


WAADVENTISTA WA SABATO WALIO FUFUTENDE (LUKEWARM SEVENTH-DAY ADVENTISTS)


1. Nandika waraka wangu, wende karibu na mbali,
Uwafikie wenzangu, mulio kila mahali,
Ameniagiza Mungu, niwadibu kulihali,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

2. Sana mlibidiika, zile enzi za zamani,
Mkawa mnatajika, mbinguni na duniani,
Lakini mmegeuka, hamko tena makini,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

3. Mumekuwa mwasusia, kukutana Jumatano,
Isomwapo Bibilia, na kwelezwa kwa mifano,
Nayo Ijumaa pia, hamwendi kwa mkutano,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

4. Sabato inapofika, hamnazo mwajitia,
Hamwishi kushughulika, Mungu mwamkaidia,
Hivyo basi mwaruzika, kwa mbovu  zenu  tabia,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

5. Mumezowea vibaya, kuchelewa Kanisani,
Hata hamuoni haya, mwenda mapema kazini,
Baadhi yenu wambeya, hutiana midomoni,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

6. Licha ya kulimatia, kuwasili Kanisani,
Kelele huwapigia, walowahi Ibadani,
Mukichoka husinzia, na kwenda usingizini,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

7. Ibadani mkitoka, mwafululiza nyumbani,
Mkiwa na uhakika, hamurudi Kanisani,
Huzidi kuhangaika, Siku ilo ya Manani,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

8. Ijapo kutoa zaka, pamwe na dhabihu zenu,
Mikono yenu birika, mwampa Mola kununu,
Mkahiniwa baraka, na kukosa nyingi tunu,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

9. Sinayo chuki na mtu, na mtu sina kinyongo,
Bali naisafi kutu, ya nyoyo na zenu bongo,
Kunoa silaha butu, za kiroho ndilo lengo,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.

10. Nahitimisha shauri, shairi nafupiliza,
Likiwa refu si zuri, kusoma na kusikiza,
Hapa basi nahiyari, beti kumi namaliza,
Enyi watunza Sabato, chungeni wenu mwenendo.
(Mtunzi: Millicent Randa, Jericho SDA Church, NAIROBI.   Mhariri: Dennis Mbae).