Sunday 10 March 2013

Jeshurun's Mind: Mashairi

Mwenzenu Nimeemewa

Wazo hili nakutubu, Mola litakabalie,
Zangu dhambi ninatubu, naomba radhi nijalie,
Manani nipe jawabu, moyo wangu utulie,
Ipo yoyote sababu, posho usinitilie?

Nielewe e Muhibu, si eti sina imani,
Liniumba na sababu, najuwa hino yakini,
Na hali uko karibu, kwa nini nina huzuni,
Niepushie dharubu, nisifu zako hisani.

Tangu kumaliza shule, kwingi nimesaka kazi,
Nikenda huku na kule, vyeti nikatoa wazi,
Nipate faida zile, wengi wanazomaizi,
Wadai wajiri wale, u haba wangu ujuzi.

Napata ahadi tele, toka kwa wanasiasa,
Wajinadi kwa upole, wasema muda ni sasa,
Tuwache mambo ya kale, tufumbate ya kisasa,
Kwani tutasonga mbele, zikwishe dhiki kabisa.

Tupu zao zote hoja, huwezi kutekeleza,
Mali zetu wamefuja, juu yetu wajitawaza,
Kazi milioni moja, kwa vijana watangaza,
Kughilibu siwe haja, komeni kutupumbaza